Ticker

6/recent/ticker-posts

DIT YABUNI MFUMO WA UFWATILIAJI NA UDHIBITI WADUDU WAHARIBIFU KWENYE MATUNDA

CHUO Cha Teknolojia Dar es Salaam (DIT) kimefanikiwa kugundua mfumo wa ugunduzi, ufwatiliaji na udhibiti wa wadudu waharibifu jamii ya Nzi ambao kwa kiasi kikubwa hushambulia mazao na matunda yenye maganda laini kama Nyanya, Embe na matango.

Akizungumza Julai 9, 2024 katika Maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa yanayofanyika kwenye Viwanja Vya Mwalimu Nyerere, barabara ya Kilwa Jijini Dar es Salaam, Mtafiti Dkt. Mkiramweni Mbazingwa kutoka DIT, alieleza kuwa Nzi wa matunda ni tishio kubwa kwa kilimo cha bustani nchini, na kusababisha hasara ya hadi asilimia 80 ya mazao ikiwa haitadhibitiwa.

Amesema wadudu hao, hasa spishi vamizi kama ‘Bactrocera dorsalis’ wanaweza kuharibu uzalishaji wa matunda, na kuathiri matumizi ya ndani na biashara ya kimataifa.

“Mbinu za kitamaduni za ufuatiliaji, ambazo zinahusisha ukaguzi wa mwongozo wa mitego ya ‘pheromone’ ni ngumu sana, hutumia wakati na huwa na makosa.

“Hii inalazimu kubuniwa kwa mbinu bora na sahihi zaidi za kugundua na kufuatilia nzi wa matunda ili kuhakikisha hatua za kudhibiti wadudu kwa wakati na zinazofaa,” amesema Mbazingwa.

Aidha amesema kuwa DIT chini ya mradi wa ‘Adaptive Environment Monitoring Network for East Africa (AdEMNEA)’ imeupa kipaumbele mfumo ili kuonyesha umuhimu wa kutumia teknolojia katika kutatua changamoto mbalimbali katika sekta ya kilimo.

Amesema AdEMNEA ni mradi wa miaka mitano unaofadhiliwa na Shirika la Ushirikiano wa Maendeleo la Norway (NORAD) chini ya ushirikiano na Chuo Kikuu cha Makerere, Uganda, Chuo Kikuu cha Yuda, Sudan Kusini, Chuo Kikuu cha Bergen na Chuo Kikuu cha Teknolojia cha Norway.

Ameeleza kuwa mradi huo ulianza mwaka 2021 ukilenga kudhibiti wadudu waharibifu wa mazao nchini.

“Mfumo wa kutambua na kufuatilia kiotomatiki wa inzi wa matunda hutumia teknolojia mbalimbali kama vile utambuzi wa picha na akili ya bandia ili kuwabaini, na kuwadhibiti wasisababishe uharibifu.

“Mfumo huu ni wa mtego unaendeshwa na nishati ya jua, una kemikali ya ‘pheromone’ ambayo inaweza kuwavuta wadudu hadi eneo la mita 100 kutoka uliko, una mechanising ya injini ambayo inaweza kuzungusha msingi wa mtego ili kumwaga wadudu au kuwaweka kwenye sehemu ya chini ya kontena kwa kuhifadhi,” amesema

Pamoja na hayo amesema mfumo huo unaweza kufuatilia mara kwa mara idadi ya nzi wa matunda waliokamatwa, na hivyo kupunguza hitaji la kutembelea maeneo ulikotegwa na kuwezesha ukusanyaji na uchambuzi wa data katika wakati halisi.

Amesema kwa kutumia teknolojia hiyo mfumo wa ugunduzi wa kiotomatiki unatoa taarifa sahihi na kwa wakati unaofaa ambazo zinaweza kuwafahamisha wakulima, maofisa wa kilimo na watafiti, kuwezesha mikakati madhubuti zaidi ya kudhibiti wadudu.

Post a Comment

0 Comments