Ticker

6/recent/ticker-posts

KINANA AWASHAURI VIONGOZI WA CCM KUZINGATIA MAADILI

Na Said Mwishehe,Mpanda

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Abdulrahman Kinana amewashauri viongozi wa Chama hicho katika ngazi mbalimbali kuzingatia maadili kwa kauli,vitendo na mwonekano.

Kinana ameyaeleza hayo leo Julai 11,2024 wakati akifungua Kongamano la Maadili na Malezi lililoandaliwa na Jumuiya ya Wazazi ya Chama hicho ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Wazazi na kilele chake kitakuwa Julai 13 mwaka huu mkoani Katavi

Akizungumza wakati wa Kongamano hilo Kinana amesema ni muhimu kila mwananchi kuwa na uadilifu katika maisha ya kila siku kwani ni jambo ambalo linasisitizwa hata katika vitabu vya Mwemyezi Mungu pamoja na viongozi mbalimbali.

Alifafanua kazi ya CCM ni kusimamia maadili, kazi ya Serikali ni kusimamia maadili na kwa upande wa Chama Cha Mapinduzi kumekuwa na vikao katika ngazi ya chini Hadi Taifa.

“Katika ngazi ya taifa kuna kamati ya maadili ya taifa, kamati ya maadili mkoani, wilayani na kata.Hii inadhihirisha umuhimu wa maadili ili tuwe na jamii bora inayojithamini na kujiheshimu.

“Unaposikiliza kauli mbiu mbalimbali zinazotolewa na viongozi ni tafsiri ya kuwa waaminifu.Kumekuwa na kauli za kukemea rushwa na Katiba ya CCM inasema sitatoa wala kupokea rushwa kwasababu rushwa ni audui wa haki.Kutoa rushwa unavunja uadilifu,”amesema.

“Vongozi tunatakiwa kuwa mfano bora wa maadili na hasa viongozi wa Chama Cha Mapinduzi, ni muhimu kuepuka mambo yote yanayoleta sifa mbaya kwa CCM au kuleta sifa mbaya kwa wana CCM pamoja na viongozi wa CCM.

“Tunawajibu wa kuyasimamia maaadili na maadili ni mambo yote mema na kueupka mabaya. Viongozi wa CCM tunatakiwa wakati wote kuwa mfano kwa kauli zetu na vitendo vyetu kwa maisha yetu yote."

Ameongeza kauli za viongozi ambazo wanazitoa zinadhihirisha maadili, kukemea rushwa, kukemea mambo yasiyo mema kwa jamii , kujenga udungu na mshikamano na kusaidiana

Kinana amesema hata kauli mbiu za waasisi wa Taifa hili akiwemo Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere ziliakisi umuhimu wa maadili.

“Hata leo tangu baba wa taifa afariki ni miaka 28 iliyopita lakini kauli zake zimebakia hai kwa kuwa alikuwa muadilifu.Ndio maana mpaka leo tunaendelea kunukuu kauli zake katika masuala mbalimbali.

"Sio viongozi wengi wa Afrika ambao wanakumbukwa na kufanyiwa rejea ya kauli zao kama anavyofanyiwa Mwalimu Nyerere.Sababu kubwa imetokana na uadilifu wake."

Hata hivyo amesema viongoziwa CCM wanawajibu kuendelea kuwa waadilifu kwa kauli na vitendo huku akipongeza Jumuiya ya Wazazi kuandaa kongamano hilo kubwa kwa ajili ya kuzungumzia maadili na malezi.

Post a Comment

0 Comments