Ticker

6/recent/ticker-posts

TBS WAENDELEA KUWANOA WAJASIRIAMALI MAONESHO YA 19 YA KIMATAIFA YA BIASHARA AFRIKA MASHARIKI MWANZA

Na Mwandishi Wetu Mwanza

WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Dkt. Selemani Jafo, amelitaka Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kuendeleza jitihada za kuhakikisha wajasiriamali nchini wanafikia malengo yao.

Waziri Dkt. Jafo alitoa kauli hiyo kwenye Maonesho ya 19 Kimataifa ya Biashara ya Afrika Mashariki yaliyofanyika kwenye Viwaja vya Furahisha, jijini Mwanza ambayo yalianza Septemba 6, mwaka huu na kumalizika jana (Septemba 15).

"TBS muendeleze jitihada hizo za kuwasaidia wajasiriamali ili waweze kuzalisha bidhaa zenye ubora ili washiriki kwenye kukuza uchumi wa nchi pamoja na uchumi wao," alisema Waziri Dtk. Jafo.

Kwa upande wake Afisa Uhusiano wa TBS, Neema Mtemvu alisema kupitia maonesho hayo waliweza kutembelea wajasiriamali na wafanyabiashara, kuwa sikiliza, kuwaelimisha na kuwahamasisha kuhusishana na umuhimu wa kuzalisha bidhaa zilizothibitishwa ubora na shirika hilo.

Alisema TBS wametumia maonesho hayo kutoa elimu kuhusu umuhimu wa kuzalisha bidhaa zenye ubora, utaratibu wa kupata alama hiyo hatua ambayo inasaidia kuwaondolea vikwazo vya kibiashara.

Mtemvu alisema shirika hilo litaendelea kutimiza dhamira ya Serikali ya kuhakikisha wajasiriamali wanashiriki katika kukuza uchumi wa nchi kwa kuhakikisha wanazalisha bidhaa zinazokidhi matakwa ya viwango.

Alisema dhamira ya Serikali kwenye hilo ipo wazi ambapo inagharamia gharama zote za wajasiriamali kuthibitisha ubora wa bidhaa wanazozalisha, hivyo wao wanachotakiwa ni kufika TBS wakiwa na barua ya utambulisho kutoka SIDO na baada ya hapo mchakato wa kuthibitisha ubora wa bidhaa zao unaanza mara moja

"Kwa hiyo kupitia maonesho haya tumewafikia wajasiriamali, kuwasikiliza na kutatua changamoto zao kwani elimu tunayowapa itarahisisha mawazo yao kuwa makubwa, kwani Serikali yetu imewarahisishia sana kila mwaka inatenga fedha kwa ajili ya kuwasaidia wajasiriamali wadogo na wa kati ili waweze kupata alama ya ubora". Alisema Mtemvu.

Alisema lengo la TBS ni kuhakikisha wajasiriamali na wazalishaji wa bidhaa wanazalisha bidhaa ambazo zimekidhi viwango stahiki na kulinda usalama wa walaji. Alizidi kufafanua kwamba wajasiriamali wakizalisha bidhaa zenye ubora zitaweza kupata soko ndani na nje ya nchi bila vikwazo vyovyote.

Hiyo ni kwa sababu nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) zimeingia makubaliano ambapo bidhaa ikishathibitishwa ubora na shirika la viwangola nchi husika, inaruhusiwa kwenye kuuzwa kokote bila kutakiwa kupimwa tena.

Kuhusu walaji, alisema nao wana mchango mkubwa katika kuhakikisha bidhaa hizo haziuzwi hapa nchini, hivyo kabla ya kununua bidhaa yoyote wanatakiwa kusoma taarifa zilizopo kwenye vifungashio pamoja na kujua kama hazijaisha muda wake wa matumizi.

Post a Comment

0 Comments